Laptop ya kwanza yenye skrini tatu yazinduliwa Marekani

 Kampuni inayotayarisha michezo ya kompyuta ya Razer imezindua kipakatalishi (kompyuta ya kupakata/laptop) mpya ambayo ina skrini tatu kwenye maonyesho ya teknolojia mpya mjini Las Vegas.

Kampuni hiyo imesema laptop hiyo ambayo imeundwa kupitia mradi uliopewa jina Valerie, ndiyo ya kwanza ya aina yake duniani.

Skrini zote tatu ni za kiwango cha kuonyesha pikzeli 4,000 (4k).
Zote ni za ukubwa wa inchi 17 (43cm). Skrini mbili huchomoza kila upande kutoka kwa skrini kubwa ya kati, moja kwa moja.
 Mmoja wa wachanganuzi wa teknolojia mpya amesifu sana laptop hiyo na kusema wachezaji wa michezo ya kompyuta siku hizi wamekuwa wakitafuta kompyuta za kisasa zaidi, ghali na zenye uwezo wa kipekee. Kompyuta hiyo inapozimwa na kufungwa, ina upana wa inchi 1.5.

Razer wamesema inalingana na laptop nyingi sana zinazotumiwa kwenye michezo ya kompyuta, ambao kawaida huwa kubwa kidogo kuliko kompyuta zinazotumiwa nyumbani na ofisini.

"Tulifikiria, 'Huu ni kama wendawazimu, tunaweza kufanya hivi," msemaji wa kampuni hiyo aliambia BBC.
"Jibu lilikuwa: 'Naam, tuna kichaa vya kutosha, tunaweza'."

Laptop iliyozinduliwa ni ya maonesho tu na Razer hawajasema ni lini wataanza kuunda kompyuta kama hizo za kuuza.

Project Valerie ni moja tu ya laptop za michezo ya kompyuta zilizozinduliwa kwenye maonesho ya CES.

Acer walizindua laptop kubwa ya inchi 21 ambayo inaitwa Predator 21X, ambayo inagharimu $8,999 (£7,250).
Samsung nao wamezindua laptop yao ya kwanza ya michezo iitwayo Samsung Notebook Odyssey, ambazo ni za ukubwa mara mbili - za inchi 17 na za inchi 15.

0 Comments

Je unamaoni kuhusu makala uliyoisoma dondosha maoni yako hapa